Nav bar

Jumatano, 3 Juni 2020

NAIBU WAZIRI ULEGA AAGIZA KUKAMILIKA KANUNI, KUSIMAMIA SHERIA YA UVUVI WA BAHARI KUU




Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Abdallah Ulega, amewataka watendaji wa Mamlaka ya Usimamizi wa Uvuvi wa Bahari Kuu kufanya maandalizi ya kupata kanuni bora za kusimamia Sheria ya Uvuvi wa Bahari Kuu iliyopitishwa hivi karibuni na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Akizungumza na watendaji wa mamlaka hiyo Mjini Unguja Visiwani Zanzibar akifuatana na Naibu Waziri wa Kilimo, Maliasili na Mifugo, Dkt. Makame Ali Ussi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Ulega aliwataka watendaji hao kuunda kanuni bora zitakazoenda sambamba na mfumo wa biashara kwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli anataka kuona namna ukanda wa bahari unavyosaidia kuinua uchumi wa taifa.

“Jumla ya vipengele vyote vya sheria takriban 104 tumevifanyia kazi na vipengele kama 23 ambavyo havijaguswa lakini vingine vyote vimeguswa kuendana na uchumi wa bahari ili kuwa na mchango kwa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla katika kufanya maboresho ya uvuvi na bahari kuu, rai yangu kwa mamlaka mmefanya kazi nzuri kwa utengenezaji wa sheria lazima kwenda mbio sasa ndani ya miezi miwili tuwe tumepata kanuni zitakazoenda sambamba na biashara ya leo bila kuathiri maslahi mapana ya taifa letu.” Alisema Ulega

Aliongeza kuwa matumizi ya sheria hiyo yatakayoenda sambamba na kanuni bora za utekelezaji wake zitakuwa chachu ya kuvutia uwekezaji kwa raia kutoka nje ya nchi kuja na meli zao hapa nchini na kufanya shughuli za uvuvi na wengine kuwekeza katika viwanda vya uchakataji wa samaki kwa kuwa Ukanda wa Pwani ya Bahari Hindi bado hakuna uwekezaji wa kutosha wa viwanda hivyo.

 Aidha, aliipongeza serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Rais Dkt. John Magufuli ilivyoboresha mazingira kwenye maziwa na mito hali iliyopelekea ndege za mizigo kubeba minofu ya samaki kutoka katika uwanja wa ndege wa Mwanza na kusafirisha kwenda nje ya nchi.

 Pia, Naibu Waziri Ulega alifafanua kuwa wakati watendaji wa Mamlaka ya Usimamizi wa Uvuvi wa Bahari Kuu wanaandaa kanuni za kusimamia sheria hiyo watambue kuwa ushirikiano ni muhimu katika utekezaji huo na kutokuwa na mvutano wowote kwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli na Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Dkt. Ali Mohamed Shein wanataka kuona mapinduzi makubwa katika sekta ya uvuvi.

 “Lazima mfanye kazi pamoja mshirikiane msiwe na aina yoyote ya mvutano, lazima mfanye kazi nzuri ya kushirikiana lazima taifa letu linufaike, Tanzania kwanza, tunaenda kufungua uvuvi wa bahari kuu tunaenda kufungua uchumi wa bluu tunataka uvuvi utoke kuchangia Asilimia 1.9 katika pato la taifa kusiwe na jambo la kunyoosheana vidole.” Alifafanua Ulega

Ulega akizungumza katika kikao hicho alisema ni muda muafaka kwa wavuvi hapa nchini kuondakana na uvuvi wa kuwinda bali uendane na teknolojia ya kisasa kufahamu maeneo mahsusi kwa ajili ya uvuvi ili kupunguza gharama kwa kutengwa vituo maalum vya kutolea taarifa ya maeneo yenye samaki na umbali wa kufikia maeneo hayo.

Alibainisha kuwa ni lazima uwepo mfumo wa kitaaalamu kwenye vyombo vyao vya uvuvi ili mvuvi anapotoka pwani kwenda baharini kuvua awe na uhakika wa mahali anapokwenda kuvua samaki na kuwataka watendaji hao kulifanyia kazi suala hilo haraka ili kufikia malengo ya wavuvi kunufaika zaidi kupitia sekta hiyo.

Katika hatua nyingine Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Abdallah Ulega, akiwa katika ziara maalum visiwani Zanzibar alitembelea kituo cha utotoaji wa vifaranga vya samaki, majongoo na kaa eneo la Maruhubi Mjini Unguja, ambapo alisema ipo miradi midogomidogo itakayoweza kutumika ikiwemo ya uvuvi wa samaki, majongoo na kaa ambayo ina soko kubwa duniani.

Ulega alisema uzalishaji wa bahari ndio nguzo kuu ya kukuza uchumi kwa wakaazi wa Ukanda wa Pwani wa Bahari ya Tanzania baada ya kufanikiwa katika ukuzaji viumbe maji kwenye maji baridi hivyo mapinduzi makubwa yanaelekezwa katika ukuzaji viumbe maji kwenye bahari.

 “Serikali imeamua kwa dhati bahari yetu iweze kutunufaisha na kuwa na mchango chanya wakati wa kuhamia katika uvuvi wa bahari kuu na jamii iweze kufuga na kukuza kipato katika viumbe ambavyo vinauzika na kuhitajika duniani kama kaa na majongoo bahari ambao wanahitajika katika mataifa ya nje ya nchi yetu na wamekuwa wakiuzwa kwa bei kubwa.”

Ulega alisema, juhudi hizo zinaendana na mikakati ya serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kufanya mapinduzi katika sekta ya kilimo itakayoinua jamii ya Ukanda wa Pwani kupitia miradi hiyo midogo.

"Tunafanya haya yote kwa ajili tunapata vyanzo vingi vya mapato vitakavyosaidia uchumi wa nchi pamoja na wananchi ambayo itatusaidia Tanzania kukuza maendeleo yake kwa haraka, kama ni utalii tunapongeza viongozi wetu wakuu kwa kusimamia haya na elimu hii iende mbali zaidi uzalishaji viumbe maji kwenye bahari unaweza kusababisha kuinuka kama taifa na kufanya vizuri zaidi kiuchumi na kuinua pato la taifa.”

Aliongeza kuwa licha ya kuelekea mpango wa uvuvi katika bahari kuu tayari miradi kama hiyo imeleta mageuzi makubwa katika maji baridi kwa maana ya maeneo ya maziwa na mito kwa upande wa Tanzania Bara.

Naye Naibu Waziri wa Kilimo, Maliasili na Mifugo, Dkt. Makame Ali Ussi, alisema, Zanzibar inaendelea na mpango wa uchumi wa bahari, kwa kuwa una nafasi kubwa ya kuingiza mapato ya haraka pamoja na kuwanufaisha wananchi wengi.

“Tunaelekea kwenye uchumi wa bluu unaohitaji kutunza mazingira ya bahari, ninawashauri watanzania sehemu zote za pwani watunze maeneo ya bahari kwa kutunza maeneo ya mazalia ya samaki yakiwemo matumbawe.” Alisema Ussi

Pamoja na hayo, alisema kuwa miradi hiyo ya uzalishaji wa samaki imekuwa na nafasi kubwa katika kukuza mazingira ya bahari ambayo tayari sehemu kubwa ya maeneo yanayotegemewa kwa uvuvi yameshaathirika.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Abdallah Ulega, amefanya ziara ya kikazi ya siku moja visiwani Zanzibar ikiwa ni moja ya mikakati ya serikali kuhakikisha sekta ya uvuvi inazidi kunufaisha zaidi taifa na mvuvi mmoja mmoja na kuongeza ushirikiano kati ya Tanzania Bara na Visiwani pamoja na kubadilishana uzoefu katika sekta hiyo.


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Abdallah Ulega (kushoto) akiwa ameshika jongoo bahari alipotembelea kituo cha utotoleshaji vifaranga vya samaki, majongoo bahari na kaa mjini Unguja, wakati wa ziara yake ya kikazi ya siku moja Visiwani Zanzibar.

Aliyevaa tai nyekundu ni Naibu Waziri wa Kilimo, Maliasili na Uvuvi wa SMZ Dkt. Makame Ali Ussi. (02.06.2020) 


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Abdallah Ulega (wa kwanza kulia) akishuhudia kaa, alipotembelea kituo cha utotoleshaji vifaranga vya samaki, majongoo bahari na kaa mjini Unguja, wakati wa ziara yake ya kikazi ya siku moja Visiwani Zanzibar.

Akiambatana na  Naibu Waziri wa Kilimo, Maliasili na Uvuvi wa SMZ Dkt. Makame Ali Ussi






Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Abdallah Ulega (aliyevaa koti jeusi) akipata maelezo ya ufuatiliaji wa meli zinazoingia katika maji ya Tanzania kwenye Bahari ya Hindi mara baada ya kutembelea ofisi za  Mamlaka ya Usimamizi wa Uvuvi wa Bahari Kuu visiwani Zanzibar. (02.06.2020) 



Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Abdallah Ulega (aliyesimama) akizungumza na watendaji wa Mamlaka ya Usimamizi wa Uvuvi wa Bahari Kuu (hawapo pichani) katika ofisi za mamlaka hiyo Visiwani Zanzibar, aliyekaa kulia ni Naibu Waziri wa Kilimo, Maliasili na Uvuvi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Dkt. Makame Ali Ussi. (02.06.2020) 




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni