Nav bar

Jumatatu, 28 Oktoba 2019

SERIKALI YASHTUKIA KUSUASUA KWA UENDESHAJI KIWANDA CHA TANGA FRESH




Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeshtukia kusuasua kwa uendeshaji wa kiwanda cha Tanga Fresh hali iliyolazimu kuundwa tume kufanya uchunguzi wa namna kiwanda kinavyofanya kazi ikiwemo kuchunguza mtambo unaotumika kusindika maziwa ya muda mrefu ambao unadaiwa umekuwa ukiongeza gharama ya uendeshaji wa kiwanda hicho.

Akizungumza jana (21.10.2019) katika kiwanda cha Tanga Fresh mjini Tanga, kwenye kikao kilichohusisha menejimenti ya kiwanda pamoja na wanachama wa Chama Kikuu cha Ushirika cha Wafugaji wa Ng’ombe wa Maziwa Mkoa wa Tanga (TDCU) kinachomiliki asilimia 43 ya kiwanda hicho.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega amefafanua kuwa serikali itahakikisha inachukua hatua kunusuru kiwanda kufuatia ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli alipotembelea kiwanda hicho mwaka 2017 na kuahidiwa na menejimenti kusindika maziwa lita laki moja kwa siku ambapo katika ziara hiyo Rais Magufuli aliwasaidia kupata hati iliyokuwa imekwama kwa miaka mingi, kuondoa changamoto ya wanahisa juu ya hisa zao Tume ya Ushindani (FCC) hali iliyopelekea kiwanda kuanza kujitanua na kuongeza uzalishaji wa maziwa ya muda mrefu (UHT) ingawa kiwanda kiliamua kuchukua mkopo Benki ya Biashara (NMB), unaoonekana kuwalemea na kutofanya vizuri sawa na ahadi kwa Rais Magufuli.

“Kwanza serikali imebaini manunuzi ya mtambo wa kusindika maziwa ya muda mrefu kuwa ni mtambo uliyokwishatumika na umenunuliwa kwa zaidi ya Shilingi Bilioni Sita, pia riba ya mkopo kuwa ni kubwa na kuwa mzigo, hivyo nimeagiza iundwe tume ambayo tayari Mkuu wa Mkoa wa Tanga ameiunda kuanzia leo kufanya uchunguzi wa mtambo ulionunuliwa ikiwemo fedha ya kununulia mtambo huo na utaratibu uliotumika kununulia mtambo.” Amesema Mhe. Ulega

Aidha Mhe. Ulega ameitaka bodi ya wakurugenzi wa kiwanda pamoja na wamiliki wakae pamoja na Benki ya Kilimo (TADB) kuitaka benki hiyo kununua deni hilo ili kutoa nafuu kwa kiwanda na kuondoa mzigo kwa wafugaji na kuinua kipato chao.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Tanga Bw. Martine Shigella amesema tayari timu ya wataalamu wakiwemo kutoka Taasisi ya Utafiti wa Viwanda na Maendeleo (TIRDO) imeshaundwa ili kubaini hali ya mtambo wa kusindika maziwa.

Bw. Shigella amefafanua kuwa serikali itachukua hatua kwa yeyote atakayebainika kukihujumu Kiwanda cha Tanga Fresh ikiwemo kununua mtambo wa kusindika maziwa usio na tija kwa kiwanda hicho.

Nao baadhi ya wanachama wa Chama Kikuu cha Ushirika cha Wafugaji wa Ng’ombe wa Maziwa Mkoa wa Tanga (TDCU) wamepongeza hatua zilizochukuliwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi pamoja na uongozi wa Mkoa wa Tanga kutafuta suluhu ya namna ya kuboresha Kiwanda cha Tanga Fresh ili kiweze kuongeza uzalishaji na kuwanufaisha wafugaji ambao wamekuwa wakiuza maziwa katika kiwanda hicho pamoja na kutaka kiwanda hicho kiongeze bei ya kununua maziwa kutoka kwa wafugaji hao ambao hawaridhiki na bei ya Shilingi 700 kwa lita moja.

Kikao baina ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi chini ya Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega, uongozi wa mkoa wa Tanga, menejimenti ya kiwanda cha Tanga Fresh, bodi na wamiliki wa kiwanda kinatarajiwa kuendelea hii leo (22.10.2019) ili kutafuta suluhu ya kunusuru kiwanda hicho baada ya kupata hasara kwa miaka mitatu mfululizo.


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega akizungumza na wanachama wa chama kikuu cha ushirika wa Ng’ombe wa maziwa Mkoa wa Tanga [TDCU] na kuagiza Mkuu wa Mkoa wa Tanga kuunda tume kuchunguza mtambo wa kusindika maziwa ya muda mrefu [UHT] ambao umekuwa ukikigharimu kiwanda icho pamoja na kutatua kero mbalimbali zilizopo katika ngazi ya menejimenti ya kiwanda na bodi ili kiwanda kiweze kuimarika. [21.10.2019]

Picha ya kwanza kushoto: Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega [kulia] akiwa na Mkuu wa Mkoa wa Tanga Bw. Martine Shingella mara baada ya kuwasili katika viwanja vya kiwanda cha Tanga Fresh kwa ajili ya kuzungumza na wanachama wa chama kikuu cha ushirika wa ngo’mbe wa maziwa Mkoa wa Tanga [TDCU] ili kutafuta suluhu ya kukinusuru kiwanda hicho kutokana na kupata hasara kwa miaka mitatu mfululizo na namna ya kuweka mazingira bora ya kuwawezesha wafugaji ili kunufaika kupitia uwepo wa kiwanda hicho. [21.10.2019]

Msajili wa bodi ya maziwa nchini Dkt. Sophia Mlote, Mkurugenzi wa Uzakishaji na Masoko kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Felix Nandonde na Meneja Mkuu wa kiwanda cha Tanga Fresh Bw. Michael Karata, wakijibu hoja mbalimbali zilizotolewa na wanachama wa chama Kikuu cha ushirika wa ng’ombe wa maziwa Mkoa wa Tanga [TDCU] zenye lengo la kutaka kiwanda hicho kuimarika zaidi na wafugaji waweze kunufaika kupitia zao la maziwa nchini. [21.10.2019]




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni