Nav bar

Jumanne, 29 Oktoba 2019

NAIBU WAZIRI ULEGA AZINDUA NA AHAMASISHA USHIRIKA WA WAVUVI KUJIKWAMUA KIUCHUMI



Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega amehamasisha wavuvi nchini kujiunga katika vyama vya ushirika wa wavuvi ili waweze kunufaika kiuchumi kupitia taasisi mbalimbali za kifedha.

Naibu Waziri Ulega amesema hayo katika Kijiji cha Kanyala kilichopo Halmashauri ya Wilaya ya Buchosa Mkoani Mwanza wakati akiwa katika ziara ya kutembelea Mikoa ya Kanda ya Ziwa kujionea shughuli mbalimbali za sekta ya mifugo na uvuvi na kuhamasisha wadau wa sekta ya uvuvi kujiunga na vyama vya ushirika wa wavuvi ili waweze kunufaika kiuchumi.

“Wavuvi wengi dhamana ya nyumba ni kikwazo kikubwa mnapohitaji mkopo kutoka katika mabenki lakini katika vyama vya ushirika sharti hilo halipo, vyama vya ushirika ndiyo mdhamini wenu na ukizingatia nimezindua Wavuvi Akuanti iliyoanzishwa na Benki ya Posta Tanzania (TPB) tunapokuwa na vyama imara vya ushirika mtakuwa na nguvu na kuweza kupata mikopo yenye masharti nafuu”. Alisema Mhe. Ulega

Aliongeza kuwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeweka mikakati ya lazima kuanzishwa kwa vyama vya ushirika vya wavuvi ili wadau wa sekta ya uvuvi waweze kusonga mbele kiuchumi na kubainisha vyama hivyo ni lazima kuhusisha wachakataji, mafundi wa boti na wavuvi na kwamba anataka biashara ya mazao ya samaki katika Ziwa Victoria linalochangia asilimia 60 ya mapato ya samaki nchini kuongezeka na kuchangia zaidi pato la taifa.

Naibu Waziri Ulega alibainisha kuwa kukua kwa uchumi wa wadau wa sekta ya uvuvi nchini kutakuwa chachu ya kuongezeka viwanda vya kuchakata samaki nchini huku akitaka wavuvi nchini kuwa na uwezo wa kupata mitaji ya biashara ili waweze kufanya biashara zaidi hususan katika ukanda wa Ziwa Victoria ambalo Tanzania inamiliki asilimia 51, Uganda asilimia 43 na Kenya asilimia sita.

Kwa upande wake Mratibu wa Dawati la Sekta Binafsi lililo chini ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bw. Stephen Michael alisema kazi kubwa ya dawati ni kuwaunganisha wafugaji na wavuvi na kuhakikisha wanainuka katika uwekezaji na malengo makubwa ni kuhakikisha vyama vya ushirika vya wavuvi vinapata mikopo kutoka katika taasisi za kifedha.

Naye Afisa Ushirika wa Halmashauri ya Wilaya ya Buchosa Bw. Martin Kimisha akisoma taarifa fupi ya uanzishwaji wa vyama vya ushirika wa wavuvi, alisema hadi kufikia mwezi Novemba mwaka 2019 wanatarajia kuwepo kwa vyama vitano ili waweze kunufaika ikiwa ni pamoja na kumudu uchakataji wa zao la samaki na bidhaa zake na kuyafikia masoko ya ndani na nje ya nchi.

Aidha Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Aballah Ulega akiwa mkoani Mwanza katika ziara yake ya kikazi ya siku tatu alifika katika Wilaya ya Ukerewe na kuzungumza na wakazi wa kisiwa cha Ukara ambapo aliwataka kulinda na kusimamia rasilimali za uvuvi nchini.

Mhe. Ulega alifafanua kuwa pindi wananchi hao watakapolinda rasilimali hizo watakuwa katika fursa nzuri zaidi kwa wao kunufaika na mazao ya samaki pamoja na kujiwezesha ili kujiunga katika vyama vya ushirika wa wavuvi kwa ajili ya kupata mikopo na kuboresha zaidi shughuli zao.

Aliongeza kuwa changamoto mbalimali alizozibaini katika kisiwa hicho zitatatuliwa na kuutaka uongozi wa Wilaya ya Ukerewe kuhakikisha unawakabidhi mashine za uvuvi watu wote ambao mashine zao zilikamatwa lakini walishalipia faini walizotozwa kutokana na makosa mbalimbali ya uvuvi katika Ziwa Victoria.

“Wale ambao walishalipia lakini hawajapewa mashine zao baada ya kukamatwa mashine hizo kutokana na makosa mbalimbali kwenye shughuli za uvuvi wakabidhiwe mashine zao.” Alibainisha Mhe. Ulega

Akiwa katika kisiwa hicho Mhe. Ulega aliwahamasisha pia wananchi hususan wanaohusika na shughuli za uvuvi kujiunga katika vyama vya ushirika wa wavuvi ili waweze kupata mikopo na kukuza shughuli zao.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega akizungumza na wakazi wa Kisiwa cha Ukara kilichopo Wilaya ya Ukerewe Mkoani Mwanza ambapo amewahamasisha wavuvi kujiunga katika ushirika ili waweze kujikwamua kiuchumi.


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega akibadilishana mawazo na Mkuu wa Wilaya ya Ukerewe Bw. Carmel Maghembe mara baada ya kuhitimisha ziara yake wilayani humo.

 

 




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni