Nav bar

Jumatatu, 13 Mei 2019

WAFUGAJI WAASWA KUBADILIKA KIFIKRA NA KUFUATA SHERIA




SERIKALI imewataka wafugaji nchini kubadili fikra zao na kutambua umuhimu wa kufuata sheria, taratibu na kanuni za nchi ili kujiepusha na mkono wa sheria pindi wanapoingiza mifugo yao katika hifadhi na mapori ya akiba.

Akizungumza na baadhi ya wafugaji jana (20.04.2019) katika Wilaya ya Meatu, Mkoani Simiyu, Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel amesema baadhi ya wafugaji wamekuwa wakiingiza mifugo yao katika hifadhi na mapori ya akiba, hivyo kusababisha kutokuwepo kwa mahusiano mazuri kati yao na wahifadhi kwa madai ya kuonewa ilhali wahifadhi hao wanatakeleza sheria za nchi.

“Tunatamani fikra za wafugaji wote nchini zibadilike na zianze kutambua umuhimu wa kufuata sheria, taratibu na kanuni, ndiyo msingi wa mafaniko. Niwaombe wafugaji wote nchini watambue kwamba Wizara ya Mifugo na Uvuvi itapenda wafugaji wafuate sheria, taratibu na kanuni, tukifanya hivyo tutakuwa marafiki wa wizara unapokuwa mhalifu unakuwa tena siyo mfugaji bali unakuwa mhalifu.” Alisema Prof. Gabriel.

Katibu mkuu huyo amelazimika kukutana na wafugaji hao kutokana na hivi karibuni ng’ombe kukamatwa katika Pori la Akiba la Maswa ambapo wamiliki wa ng’ombe hao wamekiri kufanya kosa na kulipa faini waliyotozwa na mahakama mara baada ya kukiri kosa na kutiwa hatiani.

“Hivi karibuni ng’ombe walikamatwa katika Pori la Akiba la Maswa, ndipo busara ikatumika kuona jambo hilo linafikia tamati ambapo wahusika wamekabidhiwa ng’ombe zao kwa kuwa busara imetumika na siyo kwamba wao wameshinda, kwa mujibu wa sheria wenzetu wa hifadhi wanachofanya ni kusimamia Sheria Namba Tano ya Mwaka 2009 ya Hifadhi ya Wanyamapori kwamba mifugo ikikamatwa inaweza kutaifishwa.” Alifafanua Prof. Gabriel.

Awali akizungumza na viongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Meatu kabla ya kuzungumza na wafugaji hao, Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel amewashukuru madiwani wa halmshauri hiyo wakiongozwa na Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Meatu Mhe. Juma Issack Mpina kwa uelewa wa hali ya juu baada ya Meneja wa Pori la Akiba la Maswa Bw. Lusato Masinde kutoa elimu na sheria iliyotumika na maamuzi yaliyotolewa na mahakama kwa wafugaji waliyoingiza mifugo katika Pori la Akiba la Maswa.

Aidha amebainisha kuwa kunapaswa kuwepo kwa mawasiliano mazuri kati ya viongozi na jamii ya wafugaji katika maeneo yote nchini ili kujenga mahusiano mazuri na kuelewa majukumu ya wasimamizi wa hifadhi na mapori ya akiba ambao wamekuwa wakisimamia sheria na kwamba hawapo kwa ajili ya kumuonea mtu yeyote.

Katika kikao na wafugaji Prof. Gabriel amewataka pia wasijichukulie sheria mkononi hata wanapokuwa wamepishana kauli na wasimamizi wa sheria kama ambavyo imekuwa ikijitokeza katika maeneo mbalimbali nchini ambapo amebainisha kuwa kwa kufanya hivyo ni kosa kubwa kisheria, huku akiwapongeza wafugaji wa Wilaya ya Meatu kwa kuwa watulivu na kuonesha ushirikiano kwa maafisa wa Pori la Akiba la Maswa baada ya kuingiza mifugo yao katika pori hilo kinyume na sheria na kutii hatua za kisheria zilizochukuliwa dhidi yao.

Akizungumza na wafugaji Katika kuhakikisha sekta ya ufugaji inaboreka katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo Wilaya ya Meatu, Mkoani Simiyu, Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel amesema wizara inahakikisha kwa juhudi zote inaboresha sekta ya ufugaji nchini yakiwemo malisho bora kwa kuwepo kwa shamba darasa katika wilaya hiyo na maeneo mengine.

Pia Prof. Gabriel amewataka wafugaji kufuga kisasa kwa kuwa na ng’ombe wanaopatikana kwa njia ya uhimilishaji ambao wamekuwa na matokeo mazuri kwa kuwa na nyama nyingi na maziwa mengi yenye ubora.

“Ukifuga wa kisasa wa ng’ombe wanaopatikana kwa njia ya uhimilishaji hautajivunia idadi ya ng’ombe ulionao bali kwa kilo na wingi wa maziwa ambao ng’ombe hao wanatoa, ambapo ng’ombe mmoja anafikia hadi kilogram 800 na tumehakikisha kama wizara wafugaji wanapata mbegu za ng’ombe bora kwa bei isiyozidi Shilingi Elfu Tano.” Alisema Prof. Gabriel

Kwa upande wake Meneja wa Pori la Akiba la Maswa Bw. Lusato Masinde amesema wapo kwa ajili ya kuwasaidia wananchi na kwamba wataendelea kusimamia sheria.

“Sisi tutaendelea kutoa elimu ili wananchi wafahamu umuhimu wa sheria zilizopo nchini ikiwemo inayohusu maeneo ya hifadhi na mapori ya akiba ili wananchi wasifanye shughuli zinazokatazwa katika maeneo hayo.” Alisema Bw. Masinde.

Amefafanua wao kama maafisa wanaolinda Pori la Akiba la Maswa wanahitaji ushirikiano kutoka kwa wananchi hususan wafugaji wa Wilaya ya Meatu ili kujiepusha na vitendo vinavyoweza kuwatia hatiani kwa kukiuka sheria za nchi ambazo wamepewa kuzisimamia.

Nao baadhi ya wafugaji walioshiriki kikao cha Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel wameomba kupata elimu zaidi juu ya uhimilishaji ili waweze kufuga ng’ombe kisasa na wenye tija kiuchumi.

Pamoja na hilo wamewaomba pia wafugaji wenzao kufuata sheria, taratibu na kanuni za nchi na kuwa karibu na viongozi wa wilaya hiyo ili waweze kufanya shughuli zao kwa kufuata maelekezo yao na kuwa na mawasiliano mazuri ambayo yatawaepusha kutojiingiza na ukiukwaji wa sheria kwa kuingiza mifugo kwenye maeneo wasiyoruhusiwa.



Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel akiwa katika matukio mbalimbali alipofanya kikao na wafugaji katika Wilaya ya Meatu, Mkoani Simiyu juu ya umuhimu wa kufuata sheria.

 


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni