Na. Fausta Njelekela, WMUV, Dodoma
Watumishi wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi wamepewa elimu na huduma za upimaji wa Magonjwa yasiyoambukiza mahala pa kazi (NCDs) ikiwa ni sehemu ya kuzuia na kudhibiti magonjwa hayo.
Zoezi hilo limefanyika Oktoba 15, 2025 katika ofisi za Wizara ya Mifugo na Uvuvi zilizopo Mji wa Serikali Mtumba Jijini Dodoma ambapo wataalamu kutoka Wizara ya Afya kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wakiwemo Chama cha Kisukari Tanzania (TDB) na Capital City Marathon walitoa huduma hiyo.
Akizungumzia huduma na elimu hiyo Mwakilishi wa Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Mkurugenzi Msaidizi Utawala, Bw. Samwel Mwashambwa amesema zoezi hilo litaongeza uelewa na kuwahamasisha watumishi kujua umuhimu wa mtindo bora wa maisha na ufuatiliaji wa afya zao.
Aidha, Bw. Mwashambwa amewashukuru wataalamu kutoka Wizara ya Afya, Chama cha Kisukari Tanzania (TDB) na Capital City Marathon kwa kutoa elimu na upimaji wa magonjwa hayo yasiyoambukiza mahala pa kazi.
Kwa upande wake Afisa Muuguzi Msaidizi kutoka Hospital ya Mkoa wa Dodoma, Bw. Rashid Anzi, amesema zoezi la upimaji wa magonjwa yasiyoambukiza mahala pa kazi limelenga kuongeza ufanisi wa kazi kwa watumishi na litaleta matokeo chanya katika kuongeza nguvu na maendeleo nchini.
"Magonjwa yatakayopimwa leo ni pamoja na kisukari, shinikizo la damu, uzito uliopitiliza na urefu." amesema Bw. Anzi.
Naye, Afisa Uvuvi Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bi. Upendo Hamidu amesema swala la kupima magonjwa yasiyoambukiza mahala pa kazi ni muhimu kwani linamfanya mtumishi kuelewa hali halisi ya Afya yake na kuweza kuongeza ufanisi katika kazi yake.




Hakuna maoni:
Chapisha Maoni