Nav bar

Jumamosi, 24 Julai 2021

WAWEKEZAJI VITALU VYA NARCO WATAKIWA KUFUATA TARATIBU ZA MIKATABA.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Mashauri Ndaki amewataka wawekezaji kwenye vitalu vya Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) kufuata taratibu zilizowekwa kulingana na mikataba yao.

 

Ndaki ameyasema hayo leo (09.07.2021) wilayani Misenyi Mkoa wa Kagera wakati alipotembelea Ranchi ya Mabale na kuzungumza na baadhi ya wawekezaji wenye mifugo katika vitalu hivyo.

 

Waziri Ndaki amesema kumekuwepo na tabia ya baadhi ya wawekezaji kuchukua vitalu na kutovitumia kama ilivyoelekezwa kwenye mikataba kitu ambacho kinasababisha maeneo kuwa mapori na kuvamiwa na watumiaji wengine wa ardhi.

 

Wizara kupitia NARCO imejipanga kuhakikisha wafugaji wanapata maeneo ya vitalu kwa ajili ya kufugia kitu ambacho kitasaidia kuondokana na tatizo la malisho na kupunguza migogoro ya ardhi kati ya wafugaji na watumiaji wengine.

 

“Hivyo wizara kwa sasa imejipanga kuhakikisha wawekezaji katika vitalu wanatumia maeneo hayo kwa malengo yaliyokusudiwa ikiwa ni pamoja na kuhakikisha wanalipa kodi kwa wakati,” alisema Waziri Ndaki.

 

Vilevile alisema kuwa wizara kwa sasa inaiona NARCO kama ni sehemu ya kotokea kwani kupitia kampuni hiyo wizara itaweza kuongeza ukusanyaji wa mapato na kuongeza kipato wa wafugaji.

 

Akiwa katika Ranchi hiyo Waziri Ndaki amemtaka mwekezaji wa Kampuni ya Chobo Investment kuachia eneo analolimiliki kwa sasa wakati akiendelea kujipanga ili wawekezaji wengine ambao tayari wanayo mifugo waweze kulitumia. Aidha, amemuhakikishia mwekezaji huyo kuwa atapewa eneo kwenye Ranchi nyingine ikiwa atafuata masharti ya mkataba wa NARCO.

 

Vilevile kutokana na changamoto iliyoibuliwa kuhusu muda mfupi wa ukodishaji vitalu, Waziri Ndaki amewaagiza NARCO kuangalia uwezekano wa kuongeza muda wa mikataba ya muda mfupi ili iwe ni ya miaka mitano badala ya mwaka mmoja wa sasa.

 

Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayesimamia sekta ya Mifugo, Prof. Elisante Ole Gabriel amesema wizara imejipanga kuhakisha uzalishaji wa Mifugo na mazao yake unaongezeka na kuhakikisha wawekezaji katika sekta wanasaidiwa ili wasikwame katika uwekezaji wao.

 

Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Misenyi, Katibu Tawala wa Wilaya hiyo, Abdallah Mayomba amesema kuwa uwepo wa Ranchi katika Wilaya hiyo umesaidia sana kupunguza migogoro ya ardhi lakini pia imesaidia kupunguza tatizo la malisho ambalo lilikuwa linawasumbua wafugaji.

 

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wawezekaji hao wamemueleza waziri kuwa bado wanahitaji maeneo kwa ajili ya kufugia na kuwa wanaishukuru serikali kupitia NARCO kwa ajili ya kutenga maeneo hayo na kuwashushi gharama ya ukodishaji wa vitalu.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki (Mb) akiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi kutoka wizarani na wawekezaji wa vitalu mara baada ya kumalizika kwa kikao kilichofanyika kwenye moja ya kitalu katika Ranchi ya Mabale wilayani Misenyi Mkoa wa Kagera. (09.07.2021)


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki (Mb) aliyesimama katikati akiwa kwenye picha ya pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Meja Jenerali Charles Mbuge (wa pili kutoka kulia), Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel (wa kwanza kulia), Katibu Tawala Mkoa wa Kagera, Prof. Faustine Kamuzora (wa pili kutoka kushoto) na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO), Prof. Peter Msoffe (wa kwanza kushoto) mara baada ya kumalizika kwa kikao kifupi kilichofanyika kwenye ofisi ya Mkuu wa Mkoa. (09.07.2021)

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki (Mb) akizungumza na wawekezaji waliochukua vitalu katika Ranchi ya Mabale wilayani Misenyi Mkoa wa Kagera ambapo amewaagiza kuhakikisha wanayatumia maeneo hayo kwa malengo yaliyokusudiwa kwani wasipofanya hivyo watanyang’anywa na kupatiwa wawekezaji wengine. (09.07.2021)


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel akifafanua jambo wakati wa kikao cha Waziri wa Mifugo na Uvuvi na wawekezaji katika Ranchi ya Mabale wilayani Misenyi Mkoa wa Kagera ambapo pia amewaeleza kuwa wizara inamalengo ya kuhakikisha uzalishaji wa mifugo na mazao yake unaongezeka. (09.07.2021)


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki (Mb) akiwa kwenye kitalu namba 2 kinachomilikiwa na mfugaji, Primus Karokola (kulia) wakati alipotembelea kitalu hicho kuangalia mifugo iliyopo kwenye Ranchi ya Mabale wilayani Misenyi Mkoa wa Kagera. Kushoto ni Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel. (09.07.2021)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni