Nav bar

Alhamisi, 11 Machi 2021

TAARIFA ZA UTEKELEZAJI MIFUGO, UVUVI ZATINGA BUNGENI

Wizara ya Mifugo na Uvuvi leo  imewasilisha taarifa zake za utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo kwa mwaka wa fedha uliopo (2020/2021) na mikakati iliyojiwekea katika utekelezaji wa miradi kwa mwaka ujao wa fedha (2021/2022) mbele ya kamati ya kudumu ya bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kwenye moja ya kumbi za bunge jijini Dodoma.

 

Sekta ya Mifugo ndio ilikuwa ya kwanza kuwasilisha taarifa yake ambapo Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel alibainisha kuwa sekta yake iliidhinishiwa kiasi cha Shilingi bilioni 5 kwa mwaka wa fedha wa fedha uliopo likiwa ni ongezeko la takribani asilimia 60 ukilinganisha na mwaka wa fedha uliopita (2019/2020) ambapo sekta hiyo ilitengewa kiasi cha shilingi 3.

 

“Mhe. Mwenyekiti fedha hiyo ndo tumeitumia kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwa ni pamoja na ujenzi wa majosho 20 yaliyojengwa katika Halmashauri mbalimbali za wilaya, kujenga kliniki na maabara 10 za mifugo ambazo zitagharimu shilingi milioni 700 na tayari mchakato wa kuhamisha fedha umeshaanza” Amesema Prof. Ole Gabriel.

 

Prof. Ole Gabriel ameieleza kamati kuwa uwepo wa kliniki na maabara za mifugo utawasaidia wafugaji kupata huduma bora za afya ya mifugo kwenye maeneo yao na kuondokana na hali iliyopo hivi sasa ambapo wafugaji wanalazimika kusafiri umbali mrefu kupata huduma hiyo huku pia akielezea namna Sekta hiyo ilivyofanikiwa kujenga mabwawa ya kisasa ya kunyweshea mifugo ya Kimokouwa lililopo wilayani Longido, Narakauo lililopo wilayani Simanjiro na Chamakweza lililopo wilayani Chalinze. .

 

“Lakini pia Mhe. Mwenyekiti tunaendelea na Ujenzi wa Kiwanda cha kuzalisha chanjo pale Kibaha ambacho mpaka sasa ujenzi wake umefikia asilimia 90 na fedha iliyotumika ni shilingi milioni 213 kati ya shilingi milioni 600 zilizotengwa na tayari vifaa vya maabara vimeshanunuliwa” Ameongeza Prof. Ole Gabriel.

 

Nao baadhi ya wajumbe wa kamati hiyo walipata fursa ya kuchangia mambo mbalimbali yaliyopo kwenye taarifa hiyo ambapo Mbunge wa Viti Maalum (Manyara) Mhe. Yustina Rahhi aliishauri sekta hiyo kuongeza wigo wa upatikanaji wa maafisa ugani hasa kwenye mamlaka za Serikali za Mitaa ambako ndipo wanapopatikana wafugaji wengi ushauri ambao Prof. Ole Gabriel aliupokea na kuahidi kuendelea kushirikiana na Ofisi ya Rais-Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) ili kukabiliana na changamoto hiyo.

 

Kwa upande wa taarifa ya sekta ya uvuvi iliyowasilishwa mbele ya kamati hiyo, Jumla ya shilingi bilioni 13 zilitengwa ambazo zinajumuisha shilingi bilioni 6 zinazotokana na fedha za ndani na shilingi bilioni 7 zinazotokana na fedha za nje.

 

Akiwasilisha taarifa hiyo Mkurugenzi wa Sera na Mipango (Uvuvi) Dkt. Andrew Komba amesema kuwa sekta hiyo mpaka sasa imetekeleza miradi mbalimbali ikiwa ni pamoja na Ujenzi na ukarabati wa mialo 13  ya kisasa ya kupokelea samaki, kuboresha masoko matatu ya samaki na  vituo vitano vya ukuzaji viumbe maji.

 

“Mhe. Mwenyekiti, Ujenzi wa bandari ya Uvuvi upo katika hatua za awali za upembuzi yakinifu lakini pia baada ya Serikali kuamua kutobinafsisha shirika la TAFICO tayari Serikali imeshaanza ukarabati wa miundombinu ya Shirika hilo” Amesema Dkt. Komba.

 

Aidha Dkt. Komba ameiambia kamati kuwa Sekta yake  ilipokea fedha za mradi wa Usimamizi Shirikishi wa Uvuvi kusini mwa bahari ya Hindi (Swiofish) ambapo fedha zilizotengwa kwa ajili ya kutekeleza mradi huo (bilioni 6) zimetekeleza mambo mbalimbali ikiwa ni pamoja na ujenzi wa nyumba 3 za wafanyakazi mkoani Tanga na ujenzi wa maabara ya kisasa ya Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi nchini (TAFIRI) iliyopo Kunduchi jijini Dar-es-salaam.

 

“Mhe. Mwenyekiti, hata hivyo kutokana na changamoto ya kutokuwepo kwa vituo vya kutosha vya ukuzaji viumbe maji, tumeanza mchakato wa ujenzi wa kituo kikubwa cha Ukuzaji viumbe maji pale Kunduchi ambapo jumla ya shilingi bilioni 1.6 zimetengwa kwa ajili ya kazi hiyo na kwa sasa ipo kwenye hatua ya upembuzi yakinifu na tayari Wakala wa Majengo nchini (TBA) wameshaanza kazi ya kusanifu miundombinu ya kituo hicho  kisha wao ndio watasimamia ujenzi huo” Amesema Dkt. Komba.

 

Akihitimisha taarifa zilizowasilishwa na sekta zote mbili (Mifugo na Uvuvi), Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Pauline Gekul mbali na kuishukuru kamati hiyo kwa maoni na mchango walioutoa wakati wa uwasilishwaji, ameahidi kufanyia kazi changamoto zote zilizowasilishwa na wajumbe wa kamati ambapo aliwaomba kuendelea kutoa ushirikiano wa kutosha kwenye Wizara yake ili iendelee kuboresha sekta hizo hapa nchini.

 

“Hivi karibuni Mhe. Waziri aliagiza wapangaji waliokodisha vitalu afu hawavitumii wanyang’anywe vitalu hivyo ili wapewe wafugaji wengine wenye mahitaji navyo na huu ndo msimamo wa Wizara kwa sasa kwa hiyo waheshimiwa wajumbe wa kamati, ninawahakikishia Wizara yetu itaendelea kuboresha maeneo mbalimbali ambayo awali yalikuwa ni changamoto kwa wafugaji au wavuvi” Amehitimisha Mhe. Gekul.


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Pauline Gekul akifafanua moja ya hoja zilizowasilishwa na wajumbe wa kamati ya kudumu ya Kilimo, Mifugo na Maji muda mfupi baada ya kuwasilishwa kwa taarifa ya Wizara yake kuhusu utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo kwa mwaka wa huu fedha (2020/2021) leo (09.03.2021) katika moja ya kumbi za bunge jijini Dodoma.

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel akiwasilisha taarifa ya miradi ya maendeleo iliyotekelezwa na sekta yake kwa mwaka huu wa fedha (2020/2021) mbele ya kamati ya Kudumu ya bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji leo (09.03.2021) kwenye moja ya kumbi za bunge jijini Dodoma.

Mkurugenzi wa Sera na Mipango (Uvuvi) Dkt. Andrew Komba akiwasilisha taarifa ya miradi ya maendeleo iliyotekelezwa na sekta yake kwa mwaka huu wa fedha (2020/2021) mbele ya kamati ya Kudumu ya bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji leo (09.03.2021) kwenye moja ya kumbi za bunge jijini Dodoma.

Baadhi ya Watendaji wa Sekta ya Uvuvi wakifuatilia michango inayotolewa na wajumbe wa kamati ya kudumu ya bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji muda mfupi baada ya Sekta za Mifugo na Uvuvi kuwasilisha taarifa kuhusu utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo kwa mwaka wa huu fedha (2020/2021) leo (09.03.2021) katika moja ya kumbi za bunge jijini Dodoma.


Baadhi ya Watendaji wa Sekta ya Mifugo  wakifuatilia michango inayotolewa na wajumbe wa kamati ya kudumu ya bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji muda mfupi baada ya Sekta za Mifugo na Uvuvi kuwasilisha taarifa kuhusu utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo kwa mwaka wa huu fedha (2020/2021) leo (09.03.2021) katika moja ya kumbi za bunge jijini Dodoma.





Hakuna maoni:

Chapisha Maoni