Wizara ya Mifugo na Uvuvi
kupitia sekta ya Uvuvi imeikabidhi kampuni ya ukandarasi ya Serikali ya Corporation
Sol eneo na mkataba wa Ujenzi wa Kituo kikubwa cha Ukuzaji wa Viumbe Maji ili
kazi hiyo ianze mara moja.
Makabidhiano hayo
yaliyofanyika jana katika kijiji cha Rubambangwe kilichopo wilaya ya Chato
mkoani Geita na Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) Dkt. Rashid
Tamatamah ambaye mbali na kubainisha kuwa mradi huo utakuwa ni mkubwa kuliko
yote hapa nchini, pia alielezea maeneo kadhaa yatakayohusiana na mradi huo.
Dkt. Tamatamah alisema kuwa
mradi huo utajumuisha ujenzi wa mabwawa yatakayokuwa na uwezo wa kutoa zaidi ya
tani 10 za samaki kwa mwaka, jengo la vitotoleshi vya samaki ambalo litakuwa na
uwezo wa kutoa vifaranga zaidi ya milioni mbili kwa mwaka, jengo dogo la
kutengeneza chakula cha samaki na eneo la kuhifadhia samaki hao.
“Lakini pia litajengwa jengo
la utawala ambalo ndani yake kutakuwa na ofisi, na ukumbi mdogo wa mikutano, jengo
la darasa kwa ajili ya kutoa mafunzo ya wiki mbili mpaka tatu kwa wakuzaji waviumbe
maji wanaohitaji kujifunza au kuongeza ujuzi, ujenzi wa bweni na ukumbi wa
chakula”, alisema Dkt. Tamatamah.
Aliongezea kuwa mradi huo
utagharimu kiasi cha shilingi bilioni 3.8 mpaka kukamilika kwake na tayari wizara
ilishalipa fidia ya shilingi milioni 42 kwa wakazi waliokuwa wakifanya shughuli
zao za kiuchumi katika maeneo hayo yenye ukubwa wa zaidi ya ekari 28.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa
Ukuzaji Viumbe Maji ambao ndio wasimamizi wakuu wa kituo hicho pindi
kitakapoanza kufanya kazi, Dkt. Nazaeli Madala alisema kuwa kituo hicho
kitakuwa ni ufumbuzi wa changamoto ya uchache wa samaki wanaopatikana kwenye
vyanzo vya asili.
“Kituo hiki kitahudumia mikoa
yote inayozunguka kanda ya ziwa na maeneo jirani na ukanda huu na
tutawafundisha wafugaji wa samaki, maafisa ugani wa fani ya ufugaji wa samaki
na pia kituo kitatumika kwa ajili ya mafunzo ya vitendo kwa wanafunzi wanaosoma
katika ngazi mbalimbali huko vyuoni”, aliongeza Dkt. Madala.
Madala alibainisha kuwa kituo
hicho kitawasaidia kupata muongozo wa kujenga vituo vingine katika maeneo
yanayozunguka Ziwa Tanganyika, Nyasa na maeneo ya Pwani lengo likiwa ni
kuhakikisha viwanda vyote vya samaki vilivyopo nchini havikosi malighafi.
Naye Afisa Mtendaji wa kijiji
cha Rubambangwe Bi. Restituta Majura alisema kuwa mradi huo utawanufaisha sana
wakazi wa kijiji hicho kwani mbali na kutoa ajira kwa wananchi watakaoshiriki
kwenye hatua ya ujenzi, pia wanatarajia kunufaika na uwepo wa barabara
itakayoelekea eneo la mradi ambayo pia inaelekea kwenye zahanati ya kijiji inayoendelea
kujengwa.
Kabla ya kuelekea kwenye eneo
la ujenzi wa kituo hicho, Dkt. Tamatamah akiwa na timu yake ya wataalam kutoka wizarani,
walifika ofisini kwa Mkuu wa Wilaya ya Chato Mhe. Charles Kabeho ambaye
aliishukuru Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kupeleka mradi huo kwenye Wilaya yake
na kuahidi kufuatilia kwa karibu hatua zote za ujenzi wa kituo hicho hadi
kitakapokamilika mnamo mwezi Oktoba 2020.
Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi), Dkt. Rashid Tamatamah (kulia) akikabidhi mkataba na michoro ya majengo ya kituo cha kukuzia viumbe maji kwa Meneja wa Kampuni ya Corporation Sol, Bw. Simeo Machibya leo wilayani Chato. (08.07.2020)
Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi), Dkt. Rashid Tamatamah (kulia) akikabidhi mkataba na michoro ya majengo ya kituo cha kukuzia viumbe maji kwa Meneja wa Kampuni ya Corporation Sol, Bw. Simeo Machibya leo wilayani Chato. (08.07.2020)
Mkuu wa Wilaya ya Chato Mhe.
Charles Kabeho akizungumza na ujumbe kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi na
taasisi ya ujenzi ya Corporation sol (hawapo pichani) uliofika ofisini kwake muda mfupi kabla ya
kuelekea kijiji cha Rubambangwe ambako kitajengwa kituo kikubwa cha kukuzia
viumbe Maji. (08.07.2020)
Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo
na Uvuvi (Uvuvi), Dkt. Rashid Tamatamah (kulia) akionesha mipaka ya eneo
kinapotarajiwa kujengwa kituo cha kukuzia viumbe hai katika kijiji cha
Rubambangwe wilayani Chato muda mfupi kabla ya kukabidhi eneo hilo kwa
mkandarasi (Corporation Sol) ili aweze kuanza ujenzi wa kituo hicho.
(08.07.2020)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni