Nav bar

Alhamisi, 4 Aprili 2019

MAKUBALIANO KATI YA SERIKALI NA BILL AND MELINDA GATES YATAKIWA KUTEKELEZWA




Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega amemuagiza Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo Prof. Elisante Ole Gabriel kufanya ufuatiliaji wa karibu kuhakikisha mikakati ambayo serikali imekubaliana na Taasisi ya Bill and Melinda Gates katika sekta ya mifugo inatekelezwa kama walivyokubaliana.

Naibu Waziri Ulega amesema hayo ofisni kwake jijini Dodoma alipotembelewa na ujumbe kutoka Taasisi ya Bill and Melinda Gates katika ofisi za wizara hiyo na kubainisha kuwa serikali inahakikikisha Mpango Mkakati wa Maendeleo ya Mifugo Tanzania unatekelezwa na kuishukuru taasisi hiyo kwa kutoa mchango mkubwa katika mpango huo.

“Sisi tuko pamoja na nyinyi na tunathamini makubaliano yetu na hatuwezi kuvunja makubaliano yetu ninawahakikishia kuwa nitamuagiza katibu mkuu afanye ufuatiliaji wa karibu sana kuhakikisha kwamba sisi tuna mikakati yetu tunayoifanya  lakini hii mikakati yote inaenda sambamba na kile tulichokubaliana.” Alisema Mhe. Ulega

Naibu Waziri Ulega pia amesema serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imekuwa ikifanya ufuatiliaji wa karibu katika sekta za mifugo na uvuvi kwa kulinda rasilimali za nchi kwa kutumia Operesheni Nzagamba na Operesheni Sangara ili kuondoa mambo yaliyokuwa yakifanywa bila utaratibu na kuisababishia serikali hasara.

“Tunafanya ulinzi wa rasilimali na kuondoa ule uholela na kuhakikisha kuwa zile sheria, taratibu na kanuni zinafuatwa sana kwa sababu hata masoko ya kimataifa yalitaka uholela usiwepo, mambo yawe katika utaratibu wa kisheria na kanuni zinazoongoza sekta.” Alisema Mhe. Ulega

Aidha Mhe. Ulega amesema Wizara ya Mifugo na Uvuvi, inahakikisha katika operesheni hizo sheria, kanuni na taratibu za sekta za mifugo na uvuvi zinafuatwa ili sekta hizo ziweze kusonga mbele kwa kumuwekea mazingira mazuri mwananchi ili aweze kufaidika na nchi iweze kuongeza pato la taifa.
Akizungumza katika kikao hicho ambacho kimehudhuriwa pia na wakuu wa idara kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo Prof. Elisante Ole Gabriel amebainisha baadhi ya mambo ambayo yanapaswa kusimamiwa ikiwemo elimu ili wafugaji waweze kunufaika kupitia sekta hiyo.

“Ningependa katika ushirikiano wetu huu tuzidi kushirikiana katika kutoa elimu kwa wafugaji wetu tuwe na ufugaji wenye tija, lakini eneo lingine la pili ni usimamizi dhidi ya magonjwa, la tatu ni kuwawezesha wafugaji wetu kiuchumi lakini la nne ni utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Maendeleo ya Mifugo Tanzania.” Alisema Prof. Gabriel

Prof. Gabriel pia ameainisha mambo mengine kuwa ni umuhimu wa kufanyika kwa tafiti, usimamizi na uhakikishaji wa uzalishaji bora wa mifugo ili sekta ya mifugo iweze kuwa na maendeleo endelevu.

Akizungumza kwa niaba ya Afisa Programu Mwandamizi wa Taasisi ya Bill and Melinda Gates katika Ukanda wa Afrika ya Mashariki Bibi Mercy Karanja, Mshauri Mwelekezi kutoka taasisi hiyo nchini Tanzania Prof. Marcellina Chijoriga amesema Taasisi ya Bill and Melinda Gates bado itaendelea kufanya kazi nchini kwa kufuata mpango wa serikali.

Aidha Prof. Chijoriga ameshukuru uongozi wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi ambao umekuwa ukitoa ushirikiano mkubwa kwa taasisi hiyo na kutoa ombi kwa uongozi wa wizara kuendelea kushirikiana na Taasisi ya Bill and Melinda Gates ili iweze kuleta matokeo chanya kwa wafugaji nchini.



Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega akiwa kwenye picha ya pamoja na maafisa kutoka Taasisi ya Bill and Melinda, Mercy Karanja (kulia) na Mshauri Mwelekezi wa taasisi hiyo Prof. Marcellina Chijoriga




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni