Nav bar

Jumanne, 8 Julai 2025

DKT. KIJAJI AKOSHWA NA UTAYARI WA WAFUGAJI KWENYE CHANJO NA UTAMBUZI

Na. Omary Mtamike

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji amewashukuru wafugaji nchini kwa utayari wao kwenye utekelezaji wa mpango wa kuboresha sekta ya Mifugo nchini hususan upande wa kampeni ya Chanjo na Utambuzi iliyoasisiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mhe. Dkt. Kijaji ametoa shukrani hizo Julai 07, 2025 kwenye ziara yake ya ukaguzi wa utekelezaji wa kampeni hiyo Wilaya ya Urambo mkoani Tabora ambapo ameonesha kufurahishwa na ushirikiano ambao wafugaji wameutoa kwa Serikali kwenye maeneo yote aliyopita.

“Serikali inawahakikishia wafugaji kuwa daima itaendelea kuboresha mazingira yenu ya ufugaji na ndio maana mmeona wenyewe jinsi Rais Samia alivyoamua kugharamia utambuzi wa Mifugo yote nchini zoezi ambalo awali lililalamikiwa kutokana na gharama zilizokuwa zinatozwa za shilingi 700 kwa ng’ombe mmoja” Amesema Mhe. Dkt. Kijaji

Akigusia changamoto ya wafugaji wengi kukosa maeneo yao ya malisho, Mhe. Dkt. Kijaji ameeleza kuwa Rais Samia ametoa maelekezo kwa Wizara yake, Ofisi ya Rais TAMISEMI na Wizara ya Ardhi kuainisha mipango ya matumizi bora ya ardhi ili wafugaji waoneshwe maeneo yao.

“Kwa hiyo kwa unyenyekevu nikuombe Mhe. Mkuu wa mkoa utusaidie kufahamu maeneo hayo na sisi Wizara tutahakikisha yanapata hati na kutambuliwa kama maeneo ya Wafugaji” Ameongeza Mhe. Dkt. Kijaji.

Ziara hiyo ya Mhe. Dkt. Kijaji iliyolenga kukagua utekelezaji wa kampeni ya kitaifa ya Chanjo na Utambuzi wa Mifugo iliyozinduliwa Wilaya ya Bariadi mkoani Simiyu Juni 16, 2025 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan itaendelea katika mkoa wa Morogoro Julai 10, 2025.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (katkati) akitoa chanjo ya mdondo wa kuku kama ishara ya kuanza kwa utekelezaji wa kampeni ya kitaifa ya Chanjo na Utambuzi wa Mifugo mkoani Tabora Julai 07,2025. Kulia ni Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa huo ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Nzega Mhe. Naipataki Tukai na kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Urambo Mhe. Khamis Mkanachi

Mkurugenzi wa huduma za Mifugo nchini Dkt. Benezeth Lutege (kulia) akimueleza Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (kushoto) namna zoezi la Chanjo na Utambuzi linavyotekelezwa muda mfupi mara baada ya kufika kwenye shamba la Mifugo la kampuni ya “Bashe Diary Farm” lililopo Wilaya ya Uyui mkoani Tabora Julai 07, 2025.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji na Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Tabora Mhe. Naipataki Tukai (kushoto) wakishuhudia zoezi la uchanjaji linavyofanyika Wilaya ya Urambo mkoani humo Julai 07, 2025.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni