Nav bar

Jumanne, 19 Juni 2018

TAHARIFA KWA UMMA KUHUSU TAHADHARI YA MLIPUKO WA UGONJWA WA HOMA WA BONDE LA UFA (RVF)



Ugonjwa wa Homa ya Bonde la Ufa (RVF) ni ugonjwa hatari kwa binadamu na mifugo hususan ng’ombe, mbuzi, kondoo na ngamia ambao husababishwa na virusi jamii ya Bunyaviridae. Wanyama huambukizwa kwa kuumwa na mbu aina ya ‘Aedes”. Binadamu hupata ugonjwa kwa kushika au kula nyama ya mnyama aliyeambukizwa na virusi vya ugonjwa huo

Katika  siku za hivi Mamlaka ya Hali ya Hewa Kenya, Shirika la Afya ya Wanyama Duniani (OIE) na Shirika la Afya  Duniani (WHO) wametoa taarifa za matukio ya ugonjwa wa  Homa ya Bonde la Ufa (RVF) Kaskazini mwa Kenya na Mashariki mwa nchi ya Rwanda. Hata hivyo Ugonjwa huo haupo hapa nchini.

Kutokana na kuwepo kwa ugonjwa huu katika nchi jirani, Wizara inatoa  maelekezo  yafuatayo kwa Halmashauri zote nchini (Idara za Mifugo, Afya na Elimu) na mikoa yote kuzingatia yafuatayo ili kuchukua tahadhari zote zinazotakiwa ili ugonjwa huu usiweze kuingia nchini.


(a)      Halmashauri zianze kutoa taarifa na elimu kwa umma, hasa kwa wadau wote wanaofanya shughuli za Mifugo, Utoaji wa huduma za Afya n.k. juu ya njia za kudhibiti maambukizi au mlipuko wa ugonjwa huu.

(b)     Halmashauri kuhimiza Wafugaji kuogesha mifugo yao mara kwa mara kwa kutumia viuatilifu (vyenye kiini cha pareto/pyrethroids) ili kudhibiti kupe, mbu, mbung’o na visumbufu wengine waenezao magonjwa. 

(c)      Kuwaagiza Wananchi kutoa taarifa haraka kwa Wataalamu wa Mifugo, Vituo vya Huduma za Afya au Vituo vya Uchunguzi wa Magonjwa ya Mifugo mara wanapoona vifo vingi vya ghafla kwa wanyama, kutupa au kuharibu mimba na wengine kuzubaa kwa homa kali.

(d)     Halmashauri kutoa elimu kwa Umma na kuhahakisha wanyama wote wanachinjiwa machinjioni na wapimwe na nyama yao pia ipimwe na Mtaalamu wa Mifugo kabla na baada ya kuchinjwa. Aidha, nyama zinunuliwe kwenye bucha au super-markets zilizoidhinishwa na sio mitaani.

(e)      Kamati za majanga/maafa za Wilaya ziimarishwe na kwa kushirikiana na Wadau wengine wafuatilie mwenendo na matukio ya magonjwa katika Wilaya zao na kutoa taarifa kwa Wizara husika


IMETOLEWA NA:


Dkt. Mary S.H.  Mashingo

KATIBU MKUU (MIFUGO)

WIZARA YA MIFUGO NA UVUVI










Hakuna maoni:

Chapisha Maoni